Tuesday, July 9, 2013

KIINGILIO MECHI YA STARS, UGANDA 5,000/-

Kiingilio cha chini katika mechi ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) itakayochezwa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani.

Viti vya kijani katika uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000 viko 19,648. Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu ambavyo viko 17,045 kiingilio ni sh. 7,000. Kiingilio kwa viti vya rangi ya chungwa ambavyo viko 11,897 ni sh. 10,000.

Viingilio vya daraja la juu ni kama ifuatavyo; VIP C yenye watazamaji 4,060 ni sh. 15,000 wakati sh. 20,000 ni kwa VIP B yenye watazamaji 4,160. VIP A yenye watazamaji 748 kiingilio chake ni sh. 30,000.

Mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya mwisho kuwania tiketi ya kucheza fainali hizo zitakazofanyika mwakani nchini Afrika itachezeshwa na mwamuzi Thierry Nkurunziza kutoka Burundi. Mechi ya marudiano itachezwa jijini Kampala kati ya Julai 26 na 28 mwaka huu.

Tiketi kwa ajili ya mechi hiyo itakayoanza saa 9 kamili alasiri zitaanza kuuzwa siku moja kabla ya mchezo (Ijumaa) katika vituo vifuatavyo; Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala na BMM Barbershop iliyoko Sinza Madukani.

Katika vituo hivyo tiketi zitauzwa katika magari maalumu. Magari hayo pia yatafanya mauzo ya tiketi uwanjani siku ya mechi.

Tunapenda kuwakumbusha watazamaji kutonunua tiketi mikononi mwa watu au katika maeneo yasiyohusika ili kuepuka kununua tiketi bandia, hivyo kukosa fursa ya kushuhudia mechi hiyo.

MIKOA YATAKIWA KUWASILISHA RATIBA COPA COCA-COLA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), linavitaka vyama vya mpira wa miguu vya mikoa kuwasilisha ratiba zao za michuano ya U15 Copa Coca-Cola kabla ya Julai 15 mwaka huu.

Ni vyama vya mpira wa miguu vya mikoa 16 pekee ambavyo ndivyo vimewasilisha TFF ratiba hizo mpaka sasa. Jumla ya mikoa 32 ya Tanzania Bara na Zanzibar inashiriki katika michuano hiyo ya umri chini ya miaka 15 kuanzia ngazi ya wilaya ambapo ngazi ya mikoa inatakiwa kuanza Julai 15 mwaka huu.

Mikoa ambayo tayari imewasilisha ratiba zao ni Arusha, Ilala, Kagera, Kaskazini Pemba, Kaskazini Unguja, Kigoma, Kinondoni, Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Mara, Mjini Magharibi, Morogoro, Singida, Tanga na Temeke.

0 maoni:

Post a Comment

WANAOTEMBELEA KWA SIKU