Friday, December 14, 2012

PONGEZI KWA UONGOZI MPYA DRFA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linaupongeza uongozi mpya wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika juzi (Desemba 12 mwaka huu) hoteli ya Mbezi Garden.

Ushindi aliopata Almasi Kasongo aliyechaguliwa kuwa Mwenyekiti pamoja na wajumbe wengine wa Kamati ya Utendaji unaonesha jinsi ambavyo wajumbe wa Mkutano Mkuu wa DRFA walivyo na imani kwao.

TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya DRFA ambayo hivi sasa ina kinara mpya, na kwamba ina changamoto kubwa ya kuhakikisha inaendesha shughuli za DRFA kwa kuzingatia katiba na kanuni.

Pia tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya DRFA chini ya Juma Simba na Kamati ya Uchaguzi ya TFF inayoongozwa na Deogratias Lyatto kwa kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa utulivu na kwa kuzingatia katiba na Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.

Safu mpya ya uongozi wa DRFA inaundwa na Kasongo (Mwenyekiti), Meba Ramadhan (Makamu Mwenyekiti), Msanifu Kondo (Katibu), Muhsin Said (Mwakilishi wa Mkutano Mkuu wa TFF), Benny Kisaka (Mwakilishi wa Klabu), Ally Hobe (Mhazini) na wajumbe Mohamed Shabani, Sunday Mwanahewa na Bakari Mapande.

CAF KUFANYA UKAGUZI WA ‘LESENI ZA KLABU’ JANUARI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) litatuma ofisa wake nchini mwezi ujao kwa ajili ya kufanya ukaguzi kwenye klabu za Ligi Kuu ya Tanzania kabla ya kutoa leseni kwa zile ambazo zitakuwa zimekidhi vigezo vilivyowekwa. Ili klabu ishiriki mashindano ya CAF ni lazima iwe na leseni hiyo.

Kwa mujibu wa CAF, ofisa huyo atakuwa nchini kuanzia Januari 7 mwakani ambapo atafanya ukaguzi huo hadi Januari 14 mwakani. Mbali ya ukaguzi katika klabu, pia ofisa huyo atakagua viwanja vitakavyotumika katika mashindano yake na hoteli ambazo timu kutoka nje zitakuwa zinafikia kabla ya mechi.

Baadhi ya masharti kabla ya klabu kupewa leseni ya CAF ni pamoja na kuwa na ofisi (physical address), uwanja wake wa mazoezi, programu ya maendeleo kwa vijana, sekretarieti ya kuajiriwa, hesabu za fedha zilizokaguliwa (audited accounts) na benchi la ufundi linaloundwa na watu wenye sifa zinazostahili.

0 maoni:

Post a Comment

WANAOTEMBELEA KWA SIKU