Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linaupongeza uongozi mpya wa Chama cha
Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) uliochaguliwa katika
uchaguzi uliofanyika juzi (Desemba 12 mwaka huu) hoteli ya Mbezi Garden.
Ushindi
aliopata Almasi Kasongo aliyechaguliwa kuwa Mwenyekiti pamoja na
wajumbe wengine wa Kamati ya Utendaji unaonesha jinsi ambavyo wajumbe wa
Mkutano Mkuu wa DRFA walivyo na imani kwao.
TFF
inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya DRFA
ambayo hivi sasa ina kinara mpya, na kwamba ina changamoto kubwa ya
kuhakikisha inaendesha shughuli za DRFA kwa kuzingatia katiba na kanuni.
Pia
tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya DRFA chini ya Juma Simba na
Kamati ya Uchaguzi ya TFF inayoongozwa na Deogratias Lyatto kwa
kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa utulivu na kwa kuzingatia katiba
na Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.
Safu
mpya ya uongozi wa DRFA inaundwa na Kasongo (Mwenyekiti), Meba Ramadhan
(Makamu Mwenyekiti), Msanifu Kondo (Katibu), Muhsin Said (Mwakilishi wa
Mkutano Mkuu wa TFF), Benny Kisaka (Mwakilishi wa Klabu), Ally Hobe
(Mhazini) na wajumbe Mohamed Shabani, Sunday Mwanahewa na Bakari
Mapande.
CAF KUFANYA UKAGUZI WA ‘LESENI ZA KLABU’ JANUARI
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) litatuma ofisa wake nchini mwezi ujao
kwa ajili ya kufanya ukaguzi kwenye klabu za Ligi Kuu ya Tanzania kabla
ya kutoa leseni kwa zile ambazo zitakuwa zimekidhi vigezo vilivyowekwa.
Ili klabu ishiriki mashindano ya CAF ni lazima iwe na leseni hiyo.
Kwa
mujibu wa CAF, ofisa huyo atakuwa nchini kuanzia Januari 7 mwakani
ambapo atafanya ukaguzi huo hadi Januari 14 mwakani. Mbali ya ukaguzi
katika klabu, pia ofisa huyo atakagua viwanja vitakavyotumika katika
mashindano yake na hoteli ambazo timu kutoka nje zitakuwa zinafikia
kabla ya mechi.
Baadhi
ya masharti kabla ya klabu kupewa leseni ya CAF ni pamoja na kuwa na
ofisi (physical address), uwanja wake wa mazoezi, programu ya maendeleo
kwa vijana, sekretarieti ya kuajiriwa, hesabu za fedha zilizokaguliwa
(audited accounts) na benchi la ufundi linaloundwa na watu wenye sifa
zinazostahili.
0 maoni:
Post a Comment