Monday, November 11, 2013

WADHAMINI KIBAO WAJITOKEZA UHURU MARATHON

Huku Spika wa Bunge, Anne Makinda akiongoza wabunge zaidi ya 100 kujisajili kwa ajili ya kushiriki mbio ndefu za Uhuru, maarufu kama Uhuru Marathon zinazotarajiwa kufanyika Dar es Salaam Desemba 8, mwaka huu tayari kampuni na taasisi kadhaa zimejitokeza kudhamini mbio hizo.

Wakati akijiandikisha kwa ajili ya kushiriki mbio hizo zenye lengo la kuwasisitiza Watanzania kuhusu umuhimu wa kutunza amani, umoja na mshikamano miongoni mwetu, Makinda alisema ni wakati wa kila Mtanzania kushiriki kwa njia moja au nyingine kupigania vitu hivyo.

“Naomba na nawasisitiza wabunge na viongozi mbalimbali kushiriki mbio hizi, kwani zina lengo zuri na lenye kuleta tija kwa Taifa letu.

“Mbio hizi zinatukumbusha ni lazima tuwe na amani, umoja na mshikamano, iwe ndani ya Bunge au hata nje, hivyo nategemea kuona wabunge wengi zaidi wakishiriki,” alisema.

Katibu wa Kamati ya Uhuru Marathon, Innocent Melleck alisema, kauli ya Spika Makinda ni kama kichocheo zaidi kwani kwa sasa kumejitokeza idadi kubwa ya kampuni, taasisi na hata watu binafsi wanaotaka kudhamini mbio hizo.

Melleck alisema, wanatarajia kutangaza wadhamini wa awali siku yoyote kuanzia kesho na kutaka wengine kuendelea kujitokeza kwa ajili ya mbio hizo.

Aidha alifafanua kuwa, fomu hizo zinatolewa kwa Sh 100,000 kwa wale watakaokimbia mbio za kilomita tatu, Sh 2,000 mbio za kilomita tano, Sh 6,000 kwa atakayeshiriki moja kati ya mbio za kilomita 21 au 42.

“Hizi mbio ni muhimu zaidi kwa ajili ya Taifa letu, hivyo ni vyema kwa Watanzania wote wakashiriki ili kuipigania amani iliyopo nchini mwetu na tumefurahishwa na mno na watu waliojitokeza kushiriki mpaka sasa.

“Kwetu sisi tunataka kuungana na Rais Jakaya Kikwete katika kuhakikisha tunakuwa sehemu ya kuleta umoja, amani na mshikamano ndani ya Tanzania na ndilo lengu la mbio hizi.”

Mratibu huyo anasema mbio za kilomita 3 zitakuwa maalumu kwa ajili ya viongozi wa kada mbalimbali, wakiwemo pia wale wa dini na zile za kilomita 5 pia zitakuwa za kuchangia kwa ajili ya watu wa mahitaji maalumu.

Uhuru Marathon ni mbio zinazosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki, hasa kutoka na lengo lake kubwa ambalo ni kutukumbusha kuhusu kulinda amani na kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwetu.

0 maoni:

Post a Comment

WANAOTEMBELEA KWA SIKU