BENKI ya NBC imetoa misaada yenye thamani ya zaidi ya sh. milioni 5.5 kwa waathirika wa milipuko ya mabomu iliyotokea katika kambi ya Jeshi la Ulinzi wa wananchi Tanzania (JWTZ) kikosi cha Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
Taarifa ya benki hiyo iliyotolewa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana na kusainiwa na Mshauri wa Mawasiliano wa NBC, Robi Matiko-Simba ilisema misaada iliyototolewa ni magodoro 100 yenye thamani ya Sh.milioni 3.5 yaliyokabidhiwa kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika ziara yake kwenye eneo hilo Jumatatu iliyopita.
Taarifa hiyo ilisema pamoja na misaada hiyo NBC iliamua magari yake yanayotoa huduma za matibabu (mobile clinics) ambazo huwa zikitoa huduma za afya bure kwa wananchi wa Dar-es-Salaam ziende kwenye maeneo yaliyoathirika na kutoa huduma hizo.
Pamoja na misaada hiyo taarifa hiyo ilisema katika kuhahakisha kuwa zoezi la kuwasaidia waathirika linafanikiwa NBC ilimdhamini mwanamuziki wa kizazi kipya MwanaFA katika tamasha lililoandaliwa na redio ya Clouds baina ya wasanii wa filamu na wasanii wa muziki kizazi kipya ambapo Benki ilimdhamini MwanaFA kwa fedha taslimu za Tanzania Sh. Milioni 2.
“NBC siku zote iko mbele kuhakikisha kuwa jamii inayoizunguka inafaidika na kusaidiwa pale matatizo yanapojitokeza, NBC imeguswa sana na janga hilo,” alisema taarifa hiyo ikimnukuu Mshauri huyo wa Mawasiliano akitoa wito kwa makampuni na taasisi nyingine kujitokeza na kusaidia wahanga hao ambao wana mahitaji makubwa ya chakula, mavazi na wengine hawana makazi yao yaliharibiwa na mabomu.





0 maoni:
Post a Comment