Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Spicenet Tanzania Ltd, Vinay Choudary (wa pili kushoto) akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo kuhusu mashindano ya Kimataifa ya mchezo wa Chess yatakayoanza Juni 14 mwaka huu jijini Dar es Salaam. Wengine kutoka kushoto ni Ofisa Michezo katika Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Benson Chacha, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Chess Tanzania, Joe Anea na mjumbe wa kamati ya chama cha chess, Emmanuel Mwaisumbe.
Raisi wa Chama cha Chess Tanzania (TACA), Geoffrey Mwanyika (wa pili kulia) akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo kuhusu mashindano ya Kimataifa ya mchezo wa Chess yatakayoanza Juni 14 mwaka huu jijini Dar es Salaam. Wengine kutoka kushoto ni Ofisa Michezo katika Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Benson Chacha, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Chess Tanzania, Joe Anea na mjumbe wa kamati ya chama cha chess, Emmanuel Mwaisumbe.
Baadhi ya wapiga picha za habari wakirekodi tukio hilo jijini Dar es Salaam leo.
Katika jitihada za kuufufua mchezo wa Chess nchini, Chama cha Chess Tanzania kwa kushirikiana na Spicenet Tanzania Limited moja ya makampuni yanayoongoza kwa kutoa huduma za intaneti hapa nchini, wameandaa mashindano ya wazi ya kimataifa yajulikanayo kama Spicenet Tanzania Open Chess Championship 2013 ambayo yatahusisha wachezaji kutoka Tanzania, Zambia, Uganda, Kenya, Msumbiji na Uingereza.
Mashindano hayo ambayo yatafanyika
kuanzia tarehe 14 hadi 16 Juni 2013, katika ukumbi wa Meru uliopo katika jingo
la Golden Jubilee Tower Mtaa wa Ohio jijini Dar es Salaam, ni ya kiwango cha
FIDE (Shirikisho la Chess Duniani) na ni moja ya mashindano magumu kabisa
yaliyowahi kuchezwa ndani ya muongo mmoja katika Afrika Mashariki.
Katika kunogesha, Bingwa
– GM Nigel Short, ambaye alikuwa ni mchezaji namba 3 duniani mwaka 1990 na
mpinzani wa Garry Kasparov, mchezaji mdogo kabisa na bingwa wa zamani wa Chess
Duniani ambaye anachukuliwa kama mchezaji bora kabisa wa wakati wote, atakuwa
mmoja wa washiriki.
Mashindano haya yanaweka
rekodi Afrika Mashariki kwa kuwa la kwanza katika historia ya Chess katika
ukanda huu kumualika Bingwa huyo. Pamoja na Nigel mwenye
cheo cha Grandmaster, mabigwa watatu wenye cheo cha International Master
watashiriki kutoka Zambia na wengine wenye cheo cha Fide Master kutoka Uganda.
Jumla ya washiriki inatazamiwa kuwa 80, huku wachezaji 50 wakitoka
Tanzania na 30 kutoka nchi za jirani.
Akizungumzia udhamini wao
kwenye mchezo huo, Mkurugenzi wa Spicenet, Vinay Choudary alisema wameamua
kuunganisha nguvu na Chama cha Chess Tanzania kuufufua mchezo huo Tanzania
katika jitihada za kuhakikisha kwamba nchi yetu inang’ara katika medani ya
michezo katika mashindano ya kimataifa.
“Tumeamua kudhamini
mchezo huu kwa sababu tunaamini kwamba tuna wachezaji wazuri ambao wanaweza
kufikia viwango vya kimataifa na kuiletea nchi yetu sifa katika michezo”
alisema Vinay akiongeza kwamba nia yetu ni kukisaidia Chama cha Chess
kuhakikisha mchezo huo unatangazwa na hatimaye kutambulishwa kwa watu wengi
kupitia shule, taasisi, vyuo vikuu na njia nyinginezo. Hii itatuhakikishia kuwa
na timu nzuri ya taifa ambayo inaweza kushiriki na kushinda katika mashindano
ya kimataifa.
Kwa upande wake,
makamu Mwenyekiti wa Chama cha Chess Tanzania, Joe Anea alisema
wanajivunia udhamini uliotolewa na Spicenet kwa mchezo huo na alielezea kuwa
msaada kama huo ni muhimu katika kuufufua na kuutangaza mchezo huo nchini.
Kuhusiana na zawadi,
Mwenyekiti alisema kutakuwa na jumla ya washindi watano ambapo mshindi wa
nafasi ya kwanza atapokea shilingi za Kitanzania 1,000,000; nafasi ya pili
shilingi 500,000; nafasi ya tatu shilingi 300,000 na nafasi za nne na tano
shilingi 100,000 kila mmoja.
Afisa wa
Baraza la Michezo la Taifa BMT Benson Chacha, amesema wakati umefika kwa watu
kuweka nguvu zaidi katika michezo mingine mbali na ile iliyozoeleka ili
kuongeza wigo wa taifa kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali ya
kimataifa. “ni muhimu wadau wakaangalia uwezekano wa kuiimarisha michezo
midogomidogo kwani ina fursa kubwa sana ya kututangaza kimataifa” alisema
Benson na kusisitiza kuwa BMT itaendelea kutoa ushirikiano wa hali na mali kwa
wadau wa michezo yote bila kubagua ili kuhakikisha kuwa nchi yetu inakuwa na
michezo mingi zaidi kwa manufaa ya wachezaji na jamii kwa ujumla.
Chess ni
mchezo wa mkakati wa watu wawili unaochezwa kwenye Ubao wa Chess wenye miraba
64 iliyopangwa katika mfumo wa nane kwa nane. Ni mchezo unaotambulika na Kamati
ya Kimataifa ya Olimpiki na kusimamiwa na Shirikisho la Dunia la Chess (FIDE)
ambalo linaandaa mashindano ya Chess Olympiad kila baada ya miaka miwili.
Katika Tanzania mchezo wa chess ulikuwa unasimamiwa
na Chama cha Chess Tanzania ambacho kilianzishwa na kusajiliwa chini ya Baraza
la Michezo la Taifa mwaka 1984, na mpaka mwaka 1998 mchezo ulikuwa ukichezwa
sana. Baada ya hapo ulipotea na hivyo mwaka 2010 ulianzishwa tena na mwaka 2012
Kamati ya Muda iliundwa kuendesha Chama cha Chess Tanzania.





0 maoni:
Post a Comment