Kocha
Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen amesema wanaipa umuhimu mkubwa mechi
ya mwisho ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia kwa lengo ni
kuhakikisha wanamaliza wakiwa wa pili katika kundi hilo.
Mechi
hiyo itachezwa Septemba 7 mwaka huu jijini Banjul, Gambia ambapo Taifa
Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premiem Lager itaondoka kesho
(Septemba 4 mwaka huu) saa 11 alfajiri kwa ndege ya Kenya Airways
kupitia Dakar, Senegal.
Kim
amesema wanataka kushinda ugenini, kwani licha ya kuwa wameshatolewa
lakini ushindi utawaongezea pointi kwa ajili ya viwango (rankings) vya
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) na pia kuepuka kuanzia
ngazi ya awali ya mechi za mchujo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON)
kwa fainali za 2015.
“Tunacheza
mechi hii tukiwa katika mazingira magumu, kwani wengi wa wachezaji wa
kikosi cha kwanza ni majeruhi. Sijawahi kukutana na hali hii tangu
nilipoanza kuifundisha Taifa Stars, lakini tumejipanga kuhakikisha
tunafanya vizuri,” amesema Kim.
Amesema
kwa mipango ya timu yake mechi hiyo ni muhimu tofauti na wengi
wanavyofikiria, na uamuzi wake wa kumwita beki Henry Joseph amezingatia
mambo mengi ya kiufundi ikiwemo nafasi anayocheza na uzoefu wa mchezaji
aliyekuwa akicheza nchini Norway katika klabu ya Kongsvinger IL.
Wachezaji
majeruhi katika kikosi hicho ni Shomari Kapombe, Kelvin Yondani, Aggrey
Morris, Salum Abubakar, Athuman Idd na John Bocco.
Vilevile
wachezaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu hawatakuwemo kwenye safari
baada ya klabu yao ya TP Mazembe kutuma taarifa Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) leo mchana ikidai ni wagonjwa.
Wachezaji
wanaoondoka kwenda Banjul ni Juma Kaseja, Mwadini Ali, Ali Mustafa,
Amri Kiemba, David Luhende, David Mwantika, Erasto Nyoni, Frank Domayo,
Haruni Chanongo, Henry Joseph, Jonas Mkude, Juma Liuzio, Khamis Mcha,
Mrisho Ngasa, Nadir Haroub, Said Dilunga, Simon Msuva na Vincent
Barnabas.
40 WAPITISHWA KUGOMBEA TFF, BODI YA LIGI
Kamati
ya Uchaguzi imepitisha majina ya waombaji 40 kati ya 58 kwa ajili ya
uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi
Tanzania (TPL Board) utakaofanyika mwezi ujao.
Waliopitishwa
katika orodha hiyo ya awali kwa upande wa Bodi ya Ligi ni Hamad Yahya
Juma (Mwenyekiti) na Said Muhammad Said Abeid (Makamu Mwenyekiti).
Kwa
upande wa Kamati ya Uendeshaji (Management Committee) ni Kazimoto
Miraji Muzo na Omar Khatib Mwindadi. Walioondolewa kwa vile si wenyeviti
wa klabu za daraja la kwanza kama kanuni zinavyotaka ni Michael Njuweni
Kaijage, Salum Seif Rupia na Silas Masui Magunguma.
Kanda
namba moja (Kagera na Geita) aliyepitishwa kuwania nafasi ya ujumbe
Kamati ya Utendaji ya TFF ni Kaliro Samson wakati Abdallah Hussein Musa
ameondolewa kwa kutojaza fomu ya uchaguzi kwa mujibu wa Kanuni za
Uchaguzi.
Jumbe
Oddessa Magati, Mugisha Galibona na Vedastus Lufano wamepitishwa
kuwania ujumbe kupitia Kanda namba mbili (Mara na Mwanza). Samwel Nyalla
ameondolewa kwa kutojaza kikamilifu fomu namba 1 ya maombi ya kugombea
uongozi wa TFF kwa kutoonesha malengo yake.
Waliopitishwa
katika Kanda namba tatu (Shinyanga na Simiyu) ni Epaphra Swain a Mbasha
Matutu wakati Stanslaus Nyongo ameondolewa kwa kukosa sifa ya uongozi
wa angalau uzoefu wa miaka mitano kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi na
Katiba ya TFF.
Kanda
namba nne (Arusha na Manyara) wamepitishwa wote watatu; ambao ni Ali
Mtumwa, Elley Simon Mbise na Omar Walii Ali. Kanda namba tano (Tabora na
Kigoma) nao wamepitishwa wote; Ahmed Idd Mgoyi na Yusuf Hamis Kitumbo.
Blassy
Kiondo amepitishwa peke yake kuwania ujumbe Kanda namba sita (Katavi na
Rukwa) huku Ayoub Nyaulingo aliondolewa kwa kutokuwa na uzoefu
uliothibitika wa miaka mitano katika uongozi wa mpira wa miguu.
Naye
Nazarius Kilungeja, Kamati ilikataa maombi yake ya kugombea ujumbe
kutokana na vitendo vyake visivyo vya kimichezo ambavyo kwa kiasi
kikubwa vilisababisha migogoro kwenye Mkoa wa Rukwa, hivyo suala lake
litawasilishwa kwa Kamati ya Maadili kwa ajili ya hatua zaidi.
Kanda
namba saba (Iringa na Mbeya) waliopitishwa ni David Samson Lugenge,
John Exavery Kiteve na Lusekelo Elias Mwanjala. Cyprian Kuyava
hakupitishwa kwa vile hana uzoefu wa uongozi kwa mujibu wa Katiba ya TFF
huku Ayoub Shaib Nyenzi akiondolewa kwa kushindwa kuthibitisha uraia
wake.
Elliud
Peter Mvella ameondolewa kwa kushindwa kuheshimu Kanuni za Uwajibikaji
wa Pamoja (collective responsibility) baada ya kushiriki kufanya uamuzi
ndani ya Kamati ya Utendaji ya TFF bila ya kutaka msimamo wake wa
kupinga uwekwe kwenye muhtasari na baadaye kuupinga uamuzi huo akiwa
kwenye uongozi wa mkoa. Suala lake limewasilishwa katika Kamati ya
Maadili kwa ajili ya hatua zaidi.
Waliopitishwa
kuwania ujumbe kupitia Kanda namba nane (Njombe na Ruvuma) ni James
Patrick Mhagama na Stanley William Lugenge wakati Kamanga Tambwe
ameondolewa kwa vile alipatikana na hatia ya kushiriki kwenye tuhumu za
rushwa kwa waamuzi na kufungiwa na TFF.
Kanda
namba tisa (Lindi na Mtwara) waombaji wote watatu wameptishwa. Waombaji
hao ni Athuman Kingome Kambi, Francis Kumba Ndulane na Zafarani Mzee
Damoder. Pia waombaji wote wa Kanda namba kumi (Dodoma na Singida),
Hussein Zuberi Mwamba, Stewart Ernest Masima na Charles Komba
wamepitishwa.
Waombaji
wanne kati ya watano wamepitishwa kwa Kanda namba 11 (Morogoro na
Pwani). Waliopitishwa ni Farid Mbarak, Geofrey Nyange, Juma Abbas Pinto
na Twahil Twaha Njoki.
Riziki
Juma Majala ameondolewa kwa vile akiwa mtendaji mkuu wa Chama cha Mpira
wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) alishindwa kusimamia Kanuni za Ligi kwa
kuruhusu timu ambayo si mwanachama wa wanachama wa COREFA kucheza ligi,
hivyo kusababisha mgogoro mkubwa kiasi cha mwananchi mmoja kufungua
kesi ya kusimamisha Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL). Suala lake
litawasilishwa Kamati ya Maadili kwa ajili ya hatua zaidi.
Kanda
namba 12 (Kilimanjaro na Tanga) wamepitishwa waombaji wote wawili.
Waombaji hao ni Davis Elisa Mosha na Khalid Abdallah Mohamed. Waombaji wawili kati ya watano wamepitishwa kuwania ujumbe kupitia Kanda namba 13 (Dar es Salaam).
Wagombea wawili kati ya watano wamepitishwa kuwania ujumbe kupitia Kanda namba 13 (Dar es Salaam). Wagombea hao ni Alex Crispine Kamuzelya na Muhsin Said Balhabou.
Walioondolewa
ni Omar Isaack Abdulkadir kutokana na vitendo vyake vya kutoheshimu na
kutotekeleza maagizo ya TFF kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi na Katiba
ya TFF. Atapelekwa katika Kamati ya Maadili kwa hatua zaidi.
Shaffii
Kajuna Dauda ameondolewa kwa kutumia nyaraka ya mawasiliano baina ya
FIFA na Rais wa TFF bila idhini na kuiweka hadharani kwenye ukurasa wake
wa mtandao wa kijamii, hivyo kukiuka maadili kwa kumiliki nyaraka
ambazo hazikuwa kwenye mamlaka yake. Suala lake linapelekwa katika
Kamati ya Maadili.
Naye
Wilfred Kidao ameondolewa kwa kutumia nyaraka za Kamati ya Utendaji ya
TFF bila ridhaa ya kamati, hivyo kukosa uadilifu. Suala lake
linawasilishwa kwenye Kamati ya Maadili kwa hatua zaidi.
Kwa
upande wa nafasi ya Makamu wa Rais, waombaji wote watatu wamepitishwa.
Waombaji hao ni Imani Omari Madega, Ramadhan Omari Nassib na Wallace
John Karia.
Athuman
Jumanne Nyamlani na Jamal Emil Malinzi wamepitishwa kuwania nafasi ya
Rais. Omari Mussa Nkwaruro ameondolewa kwa kuwasilisha cheti chenye
utata, hivyo kukiuka utashi wa Ibara ya 27(7) ya Katiba ya TFF. Pia
aliwasilisha taarifa za uongo kuhusu uzoefu na kukiuka Kanuni za
Maadili, hivyo suala lake linapelekwa Kamati ya Maadili.
Naye
Richard Julius Rukambula ameondolewa kwa hakukidhi matakwa ya kugombea
uongozi kwa mujibu wa Ibara ya 12(2)(e) ya Katiba ya TFF inayokataza
masuala ya mpira wa miguu kupelekwa katika mahakama za kawaida. Hivyo
naye anapelekwa katika Kamati ya Maadili kwa hatua stahiki.
IRINGA YAINYANYASA RUVUMA COPA COCA-COLA
Iringa
imeanza kwa kishindo michuano ya Copa Coca-Cola kwa watoto wenye umri
chini ya miaka 15 baada ya leo (Septemba 3 mwaka huu) kuitandika Ruvuma
mabao 4-0.
Hadi
mapumziko katika mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Shule ya Sekondari
Iyunga jijini Mbeya, washindi walikuwa mbele kwa mabao 2-0 yaliyofungwa
dakika ya 14 na Justin Luvanda huku Alphonce Kalinga akifunga la pili
dakika ya 43.
Mabao mengine yalifungwa na Juma Rogani katika dakika ya 49 na Luvanda akafumania tena nyavu dakika ya 59.
Hiyo ni mechi ya pili mfululizo kwa Ruvuma kupoteza ambapo ya kwanza ililala mbele ya wenyeji Mbeya kwa mabao 3-0.
0 maoni:
Post a Comment